
Na Mwandishi Wetu WAMACHINGA
Wasanii wa filamu nchini,na wadau wa siasa, Jimmy Mafufu na Chiki Mchoma wamejitokeza hadharani kulaani vikali kauli za baadhi ya wanasiasa wanazodai zinatishia amani ya nchi.
Wakizungumza na waandishi wa habari leo, Jimmy Mafufu amesema kuwa baadhi ya viongozi wa kisiasa wamekuwa wakitoa matamko yanayohamasisha uasi, jambo ambalo ni hatari kwa ustawi wa taifa. Mafufu amewapongeza pia maafisa wa usalama kwa kuchukua hatua za haraka dhidi ya matamko hayo.
Akimtaja mmoja wa viongozi hao, Mafufu alimnukuu Tundu Lissu, Mwenyekiti wa Chadema, aliyetoa kauli zinazohusishwa na uasi. Mafufu amesema vijana wa Kitanzania hawawezi kudanganyika na maneno yanayolenga kuvuruga amani na Katiba ya nchi.
“Tanzania iko shwari. Hatudanganyiki. Tuko tayari kupiga kura. Ukisikia maneno yanayolenga kuvuruga amani ya nchi yetu, sisi kama vijana hatuwezi kukaa kimya – tutapinga kwa nguvu zote,” amesema Mafufu.