
*📌 Majimbo yaendelea kufaidika na mradi wa umeme wa Vitongoji 15.*
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe Judith Kapinga amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imekamilisha kazi ya kupeleka umeme kwenye Vijiji vyote Tanzania Bara na nguvu sasa inaelekezwa kwenye vitongoji.
Mhe. Kapinga ameeleza kuwa, pamoja na kazi ya kupeleka umeme vitongojini inayoendelea sasa, Serikali ina mkakati wa kupeleka umeme kwenye Vitongoji 9,000 katika mwaka ujao wa fedha wa 2025/26.
Ameeleza hayo leo Aprili 09, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Nkansi Kusini, Mhe. Vicent Mbogo aliyeuliza ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vitongoji vilivyopo Jimbo la Nkansi Kusini.
“Kitongoji cha Lupata kilichopo Kata ya Kizumbi kitapata umeme kupitia mradi wa Vitongoji 15 vya kila Mbunge, na kitongoji cha Lwela Kata ya Mpembe kitapata umeme kupitia miradi itakayokuja”. Amesema Kapinga
Akijibu swali Mbunge wa Momba, Mhe. Condester Sichwale aliyeuliza ni upi mkakati wa Serikali wa kupeleka umeme kwenye Vitongoji vya Tarafa za Ndarambu, Msangano na Kamsambu, Mhe. Kapinga amesema Serikali inao mkakati wa kutekeleza miradi ya umeme kwenye Vitongoji na hivi sasa inatekeleza mradi wa kupeleka umeme kwenye Vitongoji 15 kwa kila Jimbo.
Ameongeza kuwa katika miradi wa Vitongoji 15 wakandarasi wamemaliza kazi za awali na sasa hivi wapo katika hatua ya kupata vifaa.