
Na Mwandishi Wetu WAMACHINGA
Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesikia kilio cha wananchi wa Bumbuli, mkoani Tanga kuhusu ujenzi wa barabara ya Soni – Bumbuli – Korogwe (km 77), kwa kiwango cha lami ambapo ameeleza kuwa ujenzi wa barabara hiyo utajengwa kwa awamu.
Akihutubia wananchi wa Wilaya ya Lushoto mkoani humo katika mkutano wa hadhara leo tarehe 24 Februari, 2025 Rais Samia ameeleza kuwa tarehe 06 Machi, 2025 Serikali itafungua zabuni ya kumtafuta Mkandarasi wa kujenga barabara hiyo.
Dkt. Samia amesisitiza kuwa ujenzi wa barabara hiyo utaanzia Soni- Bumbuli (km 22) na Kwameta – Kwashemsi (Km 9.3).
โBarabara hii mwanangu January (Mbunge wa Bumbuli) amekuwa akiililia sana, baada ya kusikia kilio chake basi nikasema tangazeni, tarehe 6 mwezi ujao tunafungua tenda kutafuta mkandarasiโ, amesema Dkt. Samia
Aidha, Dkt. Samia ameeleza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza ujenzi wa barabara ya Tanga – Pangani – Bagamoyo (km 218.2) kwa kiwango cha lami pamoja na ujenzi wa Daraja la Pangani lenye urefu wa mita 525.
Awali, Mbunge wa Jimbo la Bumbuli, January Makamba amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kibali cha barabara hiyo kutangazwa ambayo itakuwa mkombozi na kiuganisha kati ya Bumbuli na Korogwe Mkoani Tanga.
Rais Samia anaendelea na ziara yake mkoani Tanga ambapo leo ameweka jiwe la msingi la ufunguzi wa jengo la Halmashari ya wilaya ya Bumbuli na kuzungumza na wananchi wa wilaya ya Lushoto mkoani Tanga.