9 views 2 mins 0 comments

RAIS MWINYI :MIFUMO IMARA YA HAKI NI MSINGI WA KUKUZA IMANI KWA WANANCHI

In KITAIFA
February 10, 2025

Na Mwandishi Wetu WAMACHINGA



Rais wa Zanzibar  na  Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Mwinyi  ameeleza kuwa Serikali  inaelewa kwamba utekelezaji wa Sheria  kwa uadilifu  na kuwepo  kwa mifumo imara ya upatikanaji wa haki  ni msingi muhimu katika kujenga na kukuza Imani ya wananchi kwa  Serikali yao, kuleta amani na utulivu  katika nchi  pamoja na kuchochea mafanikio ya kiuchumi na kijamii.

Rais Dkt.Mwinyi ameyasema hayo katika kilele cha Maadhimisho ya wiki ya Sheria hafla iliofanyika Mahakama ya Mkoa wa Mjini Magharibi Mazizini, Wilaya ya Mjini , Mkoa wa Mjini Magharibi.

Aidha Rais Dkt.Mwinyi  amesema Serikali imekuwa ikisisitiza  umuhimu wa  Maadili kwa Watumishi wa Umma na kwa Upande wa Mahakama kwani suala la maadili lina uzito wa aina yake katika upatikanaji wa haki.

Ameeleza kuwa  miongoni mwa mambo yanayodhoofisha  misingi ya haki na utawala bora ni kuwepo kwa Vitendo vya Rushwa , Uzembe ,kukosa uwajibikaji na  ukiukwaji wa maadili.

Halikadhalika Rais Dkt.Mwinyi amewakumbusha Watendaji wa Mahakama na Wadau wake wote Umuhimu wa Kuzingatia Maadili  katika Utoaji wa haki kwa Wananchi.

Rais Dkt.Mwinyi  amesisitiza kuwa Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali  kuimarisha ustawi wa jamii na kiuchumi  kwa lengo la kuwawezesha wananchi  hususani wa kipato cha chini kuondokana na umasikini na kupiga hatua kimaendeleo  kwa mtu mmoja mmoja  na taifa kwa ujumla hivyo mafanikio ya Serikali katika ustawi wa jamii ni lazima yaendane na sekta ya sheria ikiwemo Mahakama.


Kwa upande mwingine Rais Dkt.Mwinyi amefahamisha kuwa wakati umefika kwa Mahakama kuongeza kasi ya kuwa na taratibu nyepesi za ufunguaji na utatuzi wa mashauri  zitakazotilia mkazo njia mbadala za utatuzi wa migogoro  ndani ya jamii.

Madhimisho hayo yaliambatana na Uzinduzi wa  Mwongozo wa Urejeshaji wa mali kwa Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi , Uzinduzi wa Mwongozo wa  Utoaji wa adhabu wa mwaka 2025 na kukabidhi ripoti ya Utendaji kazi wa Mahakama ya mwaka 2024 .

Akizungumza katika hafla hiyo Jaji Mkuu wa Zanzibar Khamis Ramadhani Abdalla Shaaban ameishukuru Serikali kwa  uimarishaji na ujenzi wa miundombinu ya Mahakama nchi  nzima kwani kwa kiasi kikubwa imekuwa kichocheo muhimu kwa maboresho ya utendaji wa mahakama na ufanisi katika upatikanaji wa  haki kwa wananchi.

  

/ Published posts: 1712

Ukurusa rasmi wa gazeti la Wamachinga. #sautiyawanyonge

Twitter
Youtube
Instagram