157 views 2 mins 0 comments

SIMBACHAWENE AWAONYA WANANCHI WANAOHARIBU VYANZO VYA MAJI JIMBONI KIBAKWE

In KITAIFA
July 22, 2023

Mbunge wa Jimbo la Kibakwe ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene ametoa onyo kwa wananchi wanaoharibu vyanzo vya maji huku akiutaka Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa kusimamia ipasavyo zoezi hilo.

Mhe. Simbachawene ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wananchi kwa nyakati tofauti katika Vijiji cha Changโ€™ombe na Kidenge vilivyopo katika Kata ya Luhundwa, Wilayani Mpwapwa, Mkoani Dodoma kupitia mikutano ya hadhara ya Mbunge huyo katika Vijiji vya Jimbo la Kibakwe, ikiwa ni muendelezo wa kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Mhe. Simbachawene ametoa maelekezo hayo kufuatia mwananchi mmoja kufanya shughuli za kilimo na ufugaji katika chanzo cha maji cha Igombo.



Amesema chanzo cha maji cha Igombo ni muhimu sana kwa mustakabali wa maisha ya wananchi wa Luhundwa na Kibakwe kwa ujumla hivyo kikiharibiwa kutakuwa na athari kubwa.

Mhe. Simbachawene ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa kumuondoa mara moja mwananchi huyo ili kunusuru chanzo hicho cha maji ambacho ni muhimu na tegemeo kwa wakazi wa maeneo hayo.

โ€˜โ€˜Maji ni uhai, siko tayari kuona vyanzo vya maji vikiharibiwa kwa maslahi ya watu wachache, ni lazima tuchukue hatua ili iwe funzo kwa wengineโ€ amesisitiza Mhe. Simbachawene.

Amesema athari za uharibifu wa mazingira zinagusa moja kwa moja masilahi ya wananchi wote bila kujali wewe ni nani katika jamii.

Ameongeza kuwa vyanzo vya maji visipolindwa Uongozi wao hautakuwa na maana kwani huko mbeleni watakuja kuulizwa na vizazi vijavyo.

Katika kulinda vyanzo hivyo vya maji, Mhe. Simbachawene ameiagiza Halmashauri ya Mpwapwa kuunda kikosi maalum kitachokuwa na jukumu la kulinda ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria wale wote watakaobainika kuharibu vyanzo vya maji.



Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, Mhe. George Fuime amemshukuru Mbunge huyo Mhe. Simbachawene kwa kuzungumzia ulinzi wa vyanzo vya maji na kumhakikishia kuwa atasimamia ipasavyo kwa kuhakikisha vyanzo hivyo vya maji vinalindwa.

Ameongeza kuwa yeye pamoja na timu yake ya Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa watajitahidi kadri ya uwezo wao huku akitoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano katika ulinzi wa vyanzo hivyo vya maji kwani bila maji hakuna maisha.

/ Published posts: 1215

Ukurusa rasmi wa gazeti la Wamachinga. #sautiyawanyonge

Twitter
Youtube
Instagram